Home » Tanzania » Mfalme wa Morocco Mtukufu Mohammed VI, amewasili hapa nchin

Mfalme wa Morocco Mtukufu Mohammed VI, amewasili hapa nchin

24 October 2016 | Tanzania

Mfalme wa Morocco Mtukufu Mohammed VI, amewasili hapa nchini tarehe 23 Oktoba, 2016 kwa ziara ya kiserikali ya siku tatu kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.

Mtukufu Mohammed VI na ujumbe wake ametua katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam Majira ya saa 11 Jioni na kupokelewa na mwenyeji wake Rais Magufuli ambapo amepigiwa mizinga 21 na kukagua gwaride rasmi la Jeshi la Wananchi Tanzania lililoandaliwa kwa heshima yake.

Kesho Rais Magufuli atafanya mazungumzo na mgeni wake Mtukufu Mohammed VI Ikulu Jijini Dar es Salaam, na baadaye watashuhudia utiaji saini wa mikataba ya ushirikiano katika masuala ya kiuchumi na biashara kati ya Tanzania na Morocco.

Baadaye Jioni Mtukufu Mohammed VI atashiriki dhifa ya kitaifa aliyoandaliwa na Mwenyeji wake Rais John Pombe Magufuli.

 

 

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Dar es Salaam

23 Oktoba, 2016

Ad