Home » Washirika » NIDA yashinda Tuzo Nane Nane

NIDA yashinda Tuzo Nane Nane

13 August 2016 | Washirika

Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa NIDA imeibuka Mshindi wa Kwanza kati ya Taasisi na Wizara za Serikali zinazotoa huduma kwa Jamii, wakifuatiwa na Wizara ya Maji na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali wakichukua Nafasi ya Tatu katika Maonyesho ya 23 ya Sikukuu ya Wakulima Nananane yaliyofanyika Mjini Lindi Kuanzia Tarehe 01 Agosti 2016 hadi Tarehe 10 Agosti 2016 katika Viwanja vya Ngongo wilaya ya Lindi Mjini.

Ushindi huo umetokana na kuzingatiwa kwa huduma za kiwango cha Juu zilizokuwa zikitolewa kwenye Banda la Mamlaka ya Vitambulisho ndani ya Maonyesho hayo ambapo ni pamoja na huduma za Usajili wa Awali uliohusisha uchukuaji wa Alama za kibaiologia na kupigwa picha, Ugawaji wa Vitambulisho vya Taifa kwa Wananchi waliokamilisha utaratibu mzima wa Usajili, Elimu kuhusiana na Matumizi ya Tovuti Salama na umuhimu wa Namba ya Utambulisho (NIN), muonekano mpya wa Vitambulisho vyenye saini ya Mmiliki wa Kitambulisho na saini ya mtoaji wa kitambulisho hicho, pamoja na huduma nyingine nyingi zilizohusu Utambulisho wa Raia, Mgeni Mkaazi na Mkimbizi.

Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, inawahimiza Wananchi wote kujitokeza kufanya usajili wa Vitambulisho vya Taifa, hasa Wakulima, Wafugaji, Wavuvi na Wafanya Biashara ili iwe rahisi kutambulika na kunufaika na huduma zitolewazo na Taasisi za Fedha na Kilimo Nchini ikiwemo kukopesheka kirahisi na kuongeza Mtaji na Upatikanaji wa pembejeo za kilimo za zana za Uvuvi

“Vitambulisho vya Taifa chachu ya Maendeleo ya Kilimo Mifugo na Uvuvi”

Ad