Home » Tanzania » Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa (CCM) Dkt. Magufuli, amefanya ziara ya kushitukiza katika Ofisi za Gazeti la Uhuru

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa (CCM) Dkt. Magufuli, amefanya ziara ya kushitukiza katika Ofisi za Gazeti la Uhuru

19 September 2016 | Tanzania

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 19 Septemba, 2016 amefanya ziara ya kushitukiza katika Ofisi za Gazeti la Uhuru zilizopo Mtaa wa Lumumba Jijini Dar es Salaam na kuzungumza na wafanyakazi.

Katika Mazungumzo hayo, wafanyakazi wa Gazeti la Uhuru linalomilikiwa na CCM wamelalamikia kutolipwa mishahara yao kwa miezi saba, kutotolewa kwa michango ya wafanyakazi kwa Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF), kuuzwa kwa mtambo wa kuchapisha magazeti katika hali ya kutatanisha, kutotambuliwa katika ajira kwa baadhi ya wafanyakazi, kutolipwa kwa madeni wanayozidai taasisi za Serikali na wanaostaafu kutolipwa mafao yao.

Wafanyakazi hao pia wamemueleza Dkt. Magufuli kuwa Bodi na Menejimenti ya kampuni ya vyombo vya habari vya chama inayoendesha Gazeti la Uhuru na Redio Uhuru zimeshindwa kuendesha vyombo hivyo na wamemuomba aingilie kati ili kuvinusuru vyombo hivyo ambavyo kwa sasa vina hali mbaya kutokana na kukabiliwa na madeni makubwa, na biashara yake imeshuka kwa kiasi kikubwa.

Akijibu malalamiko hayo Rais Magufuli aliyetembelea ofisi za Gazeti la Uhuru akitokea Ofisini kwake katika jengo la Makao Makuu ya chama, Ofisi Ndogo ya Lumumba Jijini Dar es Salaam amemuagiza Katibu Mkuu wa CCM Ndg. Abdulrahaman Kinana kuhakikisha mishahara yote wanayodai wafanyakazi inayofikia Shilingi Milioni 609 inalipwa ndani ya Mwezi huu wa Tisa, ameagiza kupatiwa orodha ya taasisi za Serikali zinazodaiwa na Magazeti ya Uhuru na Mzalendo, na pia ameagiza deni linalodaiwa na NSSF kutokana na kutowasilishwa kwa makato ya wafanyakazi lilipwe.

Kuhusu malalamiko dhidi ya Bodi na Menejimenti ya Kampuni hiyo, ajira za wafanyakazi, mafao kwa wastaafu, kuuzwa kwa mtambo wa kuchapisha magazeti na mazingira magumu ya kazi Dkt. Magufuli ameahidi kuyafanyia kazi.

Aidha, Dkt. Magufuli amewapongeza wafanyakazi wa Gazeti la Uhuru kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya licha ya kukabiliwa na changamoto kubwa na amewakikishia kuwa anatambua umuhimu wao na kwamba atahakikishia anaboresha hali ya chombo hicho muhimu.

Wakati huo huo, Rais Magufuli amemjulia hali Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samwel Sitta ambaye anaendelea kupata matibabu Jijini Dar es Salaam na hali yake inaendelea vizuri.

 

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Dar es Salaam

19 Septemba, 2016

 

Ad