Home » Tanzania » KATIBU MKUU WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO BW. DOTO JAMES AWATOA HOFU WATANZANIA KUHUSU DENI LA TAIFA

KATIBU MKUU WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO BW. DOTO JAMES AWATOA HOFU WATANZANIA KUHUSU DENI LA TAIFA

09 November 2017 | Tanzania

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James amewatoa hofu watanzania kuhusu ongezeko la Deni la Taifa akisisitiza kuwa Deni hilo ni himilivu.

Alikuwa akitolea ufafanuzi kuhusu baadhi ya watu na vyombo vya habari vinavyozungumzia Deni la Taifa kwa kutumia neno Deni la Taifa “linapaa”

Katibu Mkuu huyo ambaye pia ndiye Mlipaji Mkuu wa Serikali alisema kuwa Deni la Taifa ni himilivu kwa kutumia viwango vya kitaifa na kimataifa kwamba ili nchi iwe katika hatari ya kukua kwa Deni lake la Taifa inabidi lifikie asilimia zaidi ya 50 lakini kwa Tanzania kiwango cha deni hilo ni asilimia 32.

“Deni letu lingekuwa linapaa, hata Benki ya Dunia wasingekubali kutukopesha kwa maana hiyo tukitaka kukopa tutafanya hivyo kwa kuwa tuko chini katika viwango vya ukopaji kwa asilimia zaidi ya 18” alisema Bw. Doto James.

Kwa hiyo nawaomba hili mlichukue muuelimishe umma wa watanzania kwamba deni la Taifa ni stahimilivu, nchi inakopesheka vizuri.

Novemba 7, 2017, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akiwasilisha Bungeni mjini Dodoma Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa na Mwongozo wa Maanndalizi ya Mpango na Bajeti kwa Mwaka 2018/2019 alisema kuwa Deni la Taifa limefikia dola za Marekani milioni 26,115.2 mwezi Juni mwaka 2017.

Dkt. Mpango alieleza kuwa ongezeko hilo ni sawa na asilimia 17 ikilinganishwa na dola milioni 22,320.76 katika kipindi kama hicho mwaka 2016.

Alisema ongezeko hilo lilichangiwa na mikopo mipya iliyochukuliwa ili kugharamia miradi ya maendeleo kama vile: Standard Gauge Railway; Strategic Cities; mradi wa usafirishaji Dar es Salaam (DART) na kupanua upatikanaji wa maji safi Dar es Salaam.

Deni hilo la Taifa linajumuisha deni la Serikali lililofikia dola za Marekani milioni 22,443.70 na deni la sekta binafsi la dola za Marekani milioni 3,671.50. Pamoja na ongezeko hili, viashiria vyote bado vinaonesha kuwa deni la Taifa ni himilivu kwa kipindi cha muda mfupi, wa kati na mrefu huku uwiano kati ya deni na Pato la Taifa umefikia asilimia 31.2 ikilinganishwa na ukomo wa asilimia 56.

Ad