Home » Michezo » SAMATTA, AUBAMEYANG, waibuka Vinara wa Soka AFRICA

SAMATTA, AUBAMEYANG, waibuka Vinara wa Soka AFRICA

08 January 2016 | Michezo

Pierre-Emerick Aubameyang mshambuliaji wa timu ya taifa ya soka ya Gabon na klabu ya Borrussia Dortmund ya Ujerumani, ndio mchezaji bora wa mwaka 2015.

Aubameyang mwenye umri wa miaka 26 alipewa tuzo hiyo jijini Abuja jana usiku baada ya kupata alama 143 mbele ya mshambuliaji wa Manchester City na Cote Dvoire Yaya Toure aliyepata alama 136.

Andre Ayew, kutoka Ghana na anayechezea klabu ya Swansea nchini Uingereza, alikuwa wa tatu kwa alama 112.

Aubameyang anakuwa mchezaji wa kwanza kutoka Gabon kuwahi kushinda taji hili baada ya kupigiwa kura na makocha pamoja na wakurugenzi wa kiufudi kutoka barani Afrika.

Mshambuliaji huyo wa Borrussia Dortmund anaongoza kwa ufungaji wa mabao katika ligi ya Bundesliga msimu huu ,na kati ya mechi 17 alizocheza amefunga mabao 18.

Kwa upande wa wachezaji wanaocheza soka katika vlabu vya bara Afrika, Mtanzania Mbwana Samatta aliyekuwa anaichezea klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ameshinda tuzo ya mchezaji bora na anakuwa Mtanzania wa kwanza lakini pia kutoka Afrika Mashariki kunyakua taji hili.

Tuzo ya kocha bora imemwendelea aliyekuwa kocha wa Cote Dvoire Harve Renard ambaye aliisaidia nchi hiyo kunyakua taji la mataifa bingwa barani Afrika mwaka uliopita.

Timu bora ya mwaka pia ni Cote dvoire.

Klabu bora ni TP Mazembe ya DRC, kipa bora ni Robert Muteba Kidiaba pia kutoka klabu ya TP Mazembe.

Mchezaji bora wa kike ni Gaelle Engamouit kutoka Cameroon huku refarii bora akiwa ni Bakary Papa Gassama kutoka Gambia.

Ad