Home » Bunge » WABUNGE wagoma kusaini kwa kutumia vidole mara mbili kwa siku

WABUNGE wagoma kusaini kwa kutumia vidole mara mbili kwa siku

05 May 2016 | Bunge

Wabunge wameitaka Ofisi ya Bunge iwaondolee mara moja utaratibu wa kusaini kwa kutumia vidole mara mbili kwa siku kwa kuwa wao si wanafunzi.

Hoja hiyo iliwasilishwa kwa njia ya mwongozo na kuungwa mkono na wabunge wote isipokuwa mawaziri na Mbunge wa Konde, Khatib Said Haji (CUF) mjini Dodoma jana.

Katika Mwongozo wake, mbunge huyo alisema kitendo cha kutakiwa kusaini mara mbili kwa siku ni kero kwa wabunge na uonevu kwa kuwa hata Bunge limekuwa likitumia muda wa mapumziko wa wabunge kwa kazi za Bunge.

“Mheshimiwa Naibu Spika wewe mwenyewe muda mfupi umetangaza matangazo mbalimbali yanayotaka baadhi ya wajumbe wa kamati wakutane baada ya saa saba mchana, tunafanya kazi nje ya mapumziko yetu, haya haina tatizo... “...tatizo langu ni kitendo cha wabunge kutakiwa kusaini mara mbili kwa siku asubuhi na jioni, wakati mwingine tunatoka hapa saa saba, wabunge tunashughulikia mambo mpaka saa 12, mbunge anatumia muda wake wa mapumziko na ule wa kuhudhuria kikao cha jioni,” alisema Haji.

Alisema inasikitisha kuona mbunge anatolewa kwenye kazi za kujenga taifa ili aje tu asaini kwa kidole tena mara ya pili.

Alisema jambo hilo linawatatiza wabunge kwa kuwa wanajiona kama wanachukuliwa kama wanafunzi kwa kufuatiliwa kwani hata kwenye benki wafanyakazi hawasaini na kufuatiliwa kama ilivyo kwa wabunge hao.

Alifafanua kuwa kabla ya kuomba Mwongozo huo, alifanya utafiti kwenye benki mbalimbali ikiwemo Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ambao nao wana utaratibu kama huo wa Bunge lakini hakuna mahali wanapotakiwa kusaini kwa vidole mara mbili.

“Kutokana na uzito wa jambo hili naomba kutoa hoja wabunge mniunge mkono mpango huu ukome,” alisema na wabunge takribani wote walisimama ishara ya kumuunga mkono na kumpigia makofi na vigelegele.

Kwa upande wake, Naibu Spika, Dk Tulia Ackson alisema kutokana na namna wabunge hao walivyopokea suala hilo, pamoja na kwamba kikanuni jambo hilo halikutakiwa kuombewa mwongozo bado litaangaliwa.

“Hata hivyo, nifafanue kuwa kusaini mara mbili lengo lake si kuwafanya wabunge wanafunzi, ila lengo ni kutaka kujua nani wapo humu ndani (bungeni),” alisema Dk Ackson.

Ad